Kusamehe ni kutengeneza nafasi kwa ajili ya vitu vipya maishani mwetu, unaposhindwa kusamehe unazuia nafasi ya kupokea mambo mapya
Kusamehe ni kuuambia moyo kwamba japokuwa suala hili linaonekana gumu lakini kwa ajili ya baraka zangu na kupona kwangu ni lazima nisamehe
Huu nimfululizo wa makala ya Nguvu ya Msamaha kama hukusoma sehemu ya nne ya makala hii Gusa hapa
Kusamehe ni kuenda sambamba na neno la Mungu ya kale yamepita na tazama yamekuwa mapya 2 Wakorontho 5:17
Kusamehe ni kukaza mwendo ili uweze kulishika lile ambalo limeandikwa na Yesu Kristo kwa ajili ya maisha yako
Kusamehe ni kwa ajili ya baraka zako binafsi na siyo za yule aliyekukosea kwa sababu kila mtu anahesabiwa haki sawa na matendo yake mwenyewe
Katika makala ya jana tuliona inatupasa wakati mwingine kumtangazia aliyekukosea kwamba umemsamehe ili afahamu kabisa hauna kinyongo naye
Leo tuangalie mifano ya watu wawili waliotangazia watu waliowakosea msamaha hata kabla ya kuombwa msamaha
Mtu wa kwanza ni Stefano Mdo 7:54-60 inaongelea namna ambavyo aliuwawa kwa kupigwa mawe naye akaomba akasema Baba naomba upokee roho yangu
Kitu cha kushangaza na cha ajabu sana ni kwamba wakati watu wako bize kumpiga mawe yeye anatamka maneno haya mstari wa 60 " Akapiga magoti akalia kwa sauti kuu Bwana usiwahesabie dhambi hii"
Sentensi "Usiwahesabie dhambi hii" ni kuwaombea msamaha kwa Mungu na kama alishafikia hatua ya kumsihi Mungu awasamehe yeye mwenyewe tayari alikuwa ameshasamehe
Hakuna namna ambayo mtu unaweza kumuomba Mungu asamehe wakati wewe haujasamehe kwa sababu maandiko yanasema ni lazima tusamehe kwanza ndipo tupate kusamehewa
Hebu jichunguze na ujiulize kama ingekuwa ni wewe kwenye nafasi ya Stefano ingekuwaje?
Kama upo na mtu kakukosea kwa maneno tuu unashindwa kumsamehe vipi kama angekuwa anakukosea kwa maneno ya kejeli, dharau na matusi na wakati huo huo anakutwanga mawe?
Msamaha ni lazima kwa ajili ya afya yako, uhusiano wako na Mungu pamoja na wanadamu wengine
Tuangalie mfano mwingine wa Mwalimu na Simba wa Yuda Yesu Kristo Luke 23:34
Wakati wakimsulubisha Yesu Mathayo 27:39 inasema "Nao walipokuwa wakipita njiani, wakamtukana na wakitikisa vichwa vyao"
Hivyo kimsingi Bwana wetu Yesu Kristo naye alitukanwa, alidhihakiwa na kudharauliwa kwa ajili yetu
Lakini tizama Luka 23:34 inasema "Yesu akasema Baba uwasamehe kwa kuwa hawajui walitendalo...."
Tunaona pia Yesu Kristo naye anawatangazia msamaha hata kabla ya wao kuomba
Kuna mambo ya msingi ya kujifunza hapa Stefano na Yesu Kristo walikuwa wanatangaza msamaha kwa watu waliokuwa wanawauwa siyo tuu kwa ajili yao bali kwa ajili ya kuusogeza ufalme mbele
Mungu hataki hata mtu mmoja aangamie katika dhambi kwa sababu siyo kusudi la yeye kutuumba
Hata sisi leo tunapowaombea, kuwasamehe waliotuudhi Baba yetu wa mbinguni anatulipa dhawabu zaidi
Mwanamke Thamani!
No comments:
Post a Comment
Unaweza kutoa ushauri au kuwasiliana nasi kwa mafunzo zaidi, karibu sana